NINA MATARAJIO MAKUBWA MAPENDEKEZO YA TUME YA MABORESHO YA TAASISI ZA HAKI JINAI TANZANIA
Ahmed Hassan

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi amempongeza na kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi wa kuunda Tume ya maboresho ya mifumo ya taasisi za haki jinai Tanzania kuleta tija kiutendaji kwa mifumo ya hiyo kwa mahitaji ya sasa. Aliyasema hayo alipokutana na Tume ya maboresho ya mifumo ya taasisi za haki jinai Tanzania inayoongozwa na Mwenyekiti wake Jaji Mkuu Mstaafu Mohamed Othman Chande.

Tume hii iliteuliwa na kuzinduliwa na Rais Dkt .Samia tarehe 30 Januari ,2023 kutathmini na kuangalia maboresho ya mifumo ya haki Jinai Tanzania.
Aidha, Dk.Mwinyi amesema ana matarajio makubwa ya mapendekezo kupitia ripoti ya tume hiyo ambayo itawasilishwa kwa Rais Dkt. Samia nakuonyesha marekebisho yanayohitajika katika mfumo mzima wa kimuundo wa taasisi za haki jinai kwa kuleta ufanisi mkubwa wa utekelezaji wa utoaji haki kiufanisi zaidi na manufaa kwa Serikali zote mbili.
Naye, Mwenyekiti wa tume hiyo Jaji Mkuu Mstaafu Mohamed Othman Chande amesema tume hiyo itazungumza na wadau mbalimbali wakiwemo wananchi, asasi za kiraia na kiserikali , pamoja na taasisi zinazoshughulikia haki jinai Jeshi la Polisi, Chuo cha Mafunzo , Mamlaka ya kudhibiti Dawa za Kulevya Zanzibar, Uhamiaji , Mahakama n.k. Pia watazuru Mikoa ya Unguja na Pemba kwa siku nne kukutana na makundi hayo.










