Habari

WAZIRI MKUU ATOA MIEZI MITATU MIRADI IKAMILIKE

0:00

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ametoa miezi mitatu kwa uongozi wa mkoa wa Songwe uhakikishe unakamilisha miradi yote ambayo ilikwishapatiwa fedha kutoka Serikali Kuu lakini bado haijakamilika hadi sasa.

“Leo ni Novemba, natoa miezi mitatu ikifika Februari 28, mwakani miradi yote ambayo fedha zilikuja tangu mwaka 2021 na haijakamilishwa iwe imekamilika. Vinginevyo, nachukua hatua kali,” amesema.

Ametoa agizo hilo leo (Jumamosi, Novemba 25, 2023) wakati akizungumza na viongozi wote wa mkoa huo kwenye kikao cha majumuisho ya ziara yake mkoani humo.

Amesema Wakurugenzi Watendaji wote waliopo ni wageni lakini wa zamani ni lazima watafute ili waje kujibu hoja. “Miradi hii haikuja hapa tu, iko nchi nzima. Kuna maeneo hata zahanati hazijaisha, kwani inahitaji mabati mangapi? Ni kwa nini haijakamilika?” amehoji.

Waziri Mkuu ambaye amemaliza ziara ya kikazi ya siku tatu, amemkabidhi Mkuu wa Mkoa huo, Dkt. Francis Michael orodha ya miradi yote ambayo bado haijakamilishwa ili aisimamie.

Akitoa mifano ya miradi hiyo wilayani Mbozi, Waziri Mkuu amesema kuna bweni la wanafunzi wenye mahitaji maalum katika shule ya msingi Lutumbi ambalo sh. milioni 80 zilitolewa tangu mwaka 2021/2022 lakini hadi leo halijaisha.

“Shilingi milioni 350 zilitolewa kwa ajili ya ujenzi wa jengo la kufulia, la upasuaji na wodi ya mama na mtoto katika kituo cha afya Itaka bado havijakamilika. Kituo cha afya Arya Nambizo kilipewa shilingi milioni 500 hakijaisha, kituo cha afya Hezya kilipata shilingi milioni 500 haijaisha na zahanati ya Chizumbi ilipata sh. milioni 50, nayo haijaisha.”

Amesema wilayani Momba kuna shule ya sekondari Ikala ambayo ilipelekewa sh. milioni 470 lakini maabara bado hazijakamilika. “Kuna kituo cha afya Msagala, kilipata sh milioni 500 lakini bado milango haijawekwa. Pia sh. milioni 500 zilitolewa kwa ajili ya ujenzi wa jengo la mama na mtoto kwenye hospitali ya wilaya hiyo lakini halijaisha. “

Back to top button